Description
Shughuli 1: Kielelezo cha uainishaji wa vitenzi
Vitenzi ni mojawapo ya makundi nane ya aina za maneno katika lugha ya Kiswahili. Ni maneno yanayorejelea vitendo vinavyofanyika au vinavyofanyiwa nomino fulani na hali za kuwa kwa vitu.
Vitenzi vinaweza kuainishwa katika makundi mbalimbali kulingana na majukumu ambayo vinatekeleza katika sentensi. Kielelezo kifuatacho kinaangazia makundi hayo tofauti.

Shughuli 2: Maana ya vitenzi visaidizi
Vitenzi visaidizi ni mojawapo ya makundi mawili kuu ya vitenzi.
Hivi ni vitenzi ambavyo ambavyo huambatanishwa na vitenzi vya aina ya kileksika katika sentensi ili kuvisaidia kuwasilisha dhana tofauti kama vile nyakati, sauti, na mtazamo wa mzungumzaji.
Vitenzi viwili vinapoandamana kwa kufuatana katika sentesi, kitenzi kile ambacho kinaweza kusimama peke yake na kuleta maana ndicho kitenzi cha kileksika. Kitenzi cha kileksika kinapoambatanishwa na kitenzi kisaidizi hurejelewa kama kitenzi kikuu.Kumbuka: Vitenzi vya kileksika ni vitenzi ambavyo vinabeba maana, na hivyo vinawezesha uwasilishaji wa nia ya sentensi.
Shughuli 3: Sifa za vitenzi visaidizi
- Dhima ya vitenzi visaidizi katika sentensi ni ya kisarufi.
- Vitenzi visaidizi hutekeleza kazi katika sentensi kama sehemu ya kishazi cha kitenzi.
- Kuwepo kwa kitenzi kisaidizi katika sentensi kunategemea kuwepo kwa kitenzi kikuu. Hapawezi kuwa na kitenzi kisaidizi pasipo na kitenzi kikuu.
- Vitenzi visaidizi hutangulia kitenzi kikuu katika sentensi.
- Kunaweza kuwa na kitenzi kisaidizi kimoja au zaidi kabla ya kitenzi cha kileksika katika sentensi.
Kumbuka: Kishazi cha kitenzi ni sehemu ya sentensi ambayo inaundwa kwa kuambatanisha kitenzi kisaidizi na kitenzi cha kileksika.
Shughuli 4: Uanishaji zaidi wa vitenzi visaidizi
Vitenzi visaidizi vinaweza kuainishwa zaidi katika makundi mawili yafuatayo:
- Vitenzi visaidizi vya modali
Aina hii ya vitenzi huwasilisha mitazamo na dhamira ya mawasiliano ya mzungumzaji. Inaonyesha iwapo anachosema mzungumzaji:
- ni kauli ya msingi
- ni swali au amri
- ni hali ya dhahania ambayo inaweza kutokea au isitokee.
Dhana zinazoweza kuwasilishwa kwa kutumia vitenzi hivi ni pamoja na; pendekezo, uwezo, wajibu, ushauri, mwaliko, ombi, hitimisho, uwezekano, ulazima, ruhusa na kutoidhini.
Matumizi ya alama za uakifishaji katika maandishi huboresha uwasilishaji wa baadhi ya dhana hizi.
- Vitenzi visaidizi vya msingi
Vitenzi hivi hutoa taarifa za ziada za kisarufi, na huonyesha jinsi ya kutafsiri kitenzi cha kileksika (kikuu) kinachofuata kwa kuwezesha:
- uwasilishaji wa nyakati tofauti za vitenzi
- ubadilishaji wa sauti za vifungu katika sentensi (amilifu/tendeshi au isoamilifu/tendaji)
- uundaji wa maswali, kauli za kusisitiza, na ukanusho.
Kumbuka: Maoni ya wazungumzaji kuhusu vitu mara nyingi hutofautiana.
Shughuli 5: Mifano ya vitenzi visaidizi vya modali katika sentensi
Ifuatayo ni mifano ya vitenzi visaidizi vya modali katika sentensi.
Kitenzi kisaidizi cha modali
Mifano ya vitenzi visaidizi vya modali katika sentensi
Mfano wa dhana
lazima
Lazima ufike pale kabla ya saa mbili.
ulazima
unaweza
Unaweza kufika pale kabla ya saa mbili?
ombi
unastahili
Unastahili kufika pale kabla ya saa mbili.
wajibu
hautaweza
Hautaweza kufika pale kabla ya saa mbili.
hitimisho
unapaswa
Unapaswa kufika pale kabla ya saa mbili.
ushauri
unaweza
Unaweza kufika pale kabla ya saa mbili.
uwezo
Kumbuka:
- Kitenzi kisaidizi lazima kiambatane na kitenzi kikuu.
- Vitenzi visaidizi hutangulia kitenzi kikuu katika sentensi.
- Baadhi ya vitenzi vinaweza kutumika kama vitenzi visaidizi au vitenzi vishirikishi. Ili kuthibitisha kwamba kitenzi fulani kimetumika kama kitenzi kisaidizi katika sentensi fulani, hakikisha kwamba kitenzi hicho kinaambatanishwa na kitenzi kikuu, wala si kijalizo.
Reviews
There are no reviews yet.